Ijumaa, 15 Januari 2016

Lowassa Atangaza Kugombea Tena Urais Mwaka 2020

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa jana alitangaza  kwamba anajiandaa kugombea tena urais utakapofika uchaguzi mkuu ujao Oktoba 2020. 
Lowassa alitangaza hayo mbele ya wafanyabiashara wa sokoni Kariakoo jijini Dar es Salaam wanaojiita Team Mabadiliko, waliokwenda kumtembelea ofisini kwake Mikocheni, Dar es Salaam.
Lowassa alisema bado anazo nguvu na kumwezesha kugombea nafasi hiyo ya juu kabisa katika uongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hatua hiyo inakuja wakati Lowassa akijipatia umaarufu zaidi kama mpambanaji mahiri kisiasa, ambaye aliingia katika kinyang’anyiro hicho kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka jana, akisimamia kambi kuu ya upinzani nchini.
Alijiunga na upinzani kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) lakini akapata kuungwa mkono na muungano wa UKAWA ulioundwa na chama hicho pamoja na Civic United Front (CUF), National League for Democracy (NLD) na NCCR-Mageuzi.
Ugombeaji wake ulikuja baada uamuzi wake mgumu wa kuhama Chama Cha Mapinduzi (CCM) alichoanzia siasa miaka ya 1980 hadi kufikia ngazi ya Waziri Mkuu, wadhifa aliouteuliwa kushika Novemba 2005 hadi Februari 2008 alipojiuzulu kufuatia shinikizo la Bunge kutokana na kashfa ya mkataba tata wa umeme wa Richmond.
Lowassa alitoa ushindani mkali katika uchaguzi mkuu kiasi cha kuaminika kuwa alipata kura za kutosha kutwaa urais, lakini Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilimtangaza mgombea wa CCM, Dk. John Magufuli kuwa mshindi. Daktari huyo wa kemia aliapishwa rasmi Novemba 5, mwaka jana.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Jumla ya Mara Iliyotazamwa