Jumatatu, 16 Machi 2015

WANAKIJIJI WAILALAMIKIA SERIKALI KUTOKANA NA SHULE YAO KUWA NA MWALIMU MMOJA WILAYANI LUDEWA.


 Mwalimu Shamim Kiyao ndiye mwalimu pekee katika shule ya msingi Kingole




majengo ya shule yamsingi Kingole



Wananchi wa kijiji cha Kingole kata ya masasi wilayani Ludewa katika mkoa wa Njombe wameitupia lawama Serikali ya wilaya kwa kushindwa kuwapeleka walimu katika shule ya msingi Kingole kwa muda wa mwaka mmoja wa 2014 hali iliyosababisha shule hiyo kushindwa kufaulisha wanafunzi wa kwenda kidato cha kwanza.

Akiongea kwa masikitiko makubwa mmoja wa wananchi hao aliyejitambulisha kwa jina la Nuru Haule alisema kuwa shule hiyo kongwe ambayo imetoa wasomi wengi katika kata ya Masasi imekuwa ikifanya vibaya kila mwaka kutokana na ukosefu wa walimu ambapo kwa mwaka 2014 ilibakiwa na mwalimu mmoja ambaye alishindwa kufanya kazi ipasavyo na kupelekea matokeo kuwa mabaya kwani kati ya watahiniwa 28 waliofaulu kujiunga na kidato cha kwanza walikuwa 2.

Bw.Haule alisema hiyo yote inatokana na wizara ya elimu kutoiwezesha idara ya elimu ukaguzi kwani mpaka sasa shule za msingi zenye walimu wakutosha ni zile za mjini na si vijijini ambako hakufikiki na wakakuzi wa elimu hali ambayo ni hatari kama shule ya kingole ambayo iko katika makao makuu ya kata kunakuwa na mwalimu mmoja  na ni kata ya kihistoria ambayo ilikuwa ni makao makuu ya chief Masasi.

“Tunashangazwa na hii hali ya kuwa na mwalimu mmoja wakati makao makuu ya wilaya shule moja ina walimu zaidi ya 20 na hali ya shule za vijijini inazidi kuwa mbaya siku hadi siku kwa mpango huu wa Serikali wa kuzisahau shule za vijijini tunategemea nini kwa vizazi vijavyo?tunaomba kuthaminiwa kama watanzania kwa kupewa haki sana na mjini kama watanzania wengine”,alisema Bw.Haule.

Naye mwalimu Shamim Kiyao ambaye ni mwalimu pekee wa shule ya msingi Kingole alisema awali shule hiyo ilikuwa na walimu watatu lakini ikatokea mmoja alikwenda masomoni na mwingine likizo ya uzazi hivyo akabaki mwalimu mmoja ndiye yeye aliyekuwa akifundisha madarasa yote saba.

Mwalimu Shamimu alisema hali ilikuwa ngumu zaidi katika tarehe za mishahara kwani ilimlazimu kufunga shule na kusafiri kufuata mshahara wilayani lakini hali ilikuwa ngumu zaidi pale alipougua kwa muda shule ilifungwa pia mpaka alipopona ndipo wanafunzi waliweza kurejea shuleni na kuendelea na masomo hivyo kufanya ufaulu kushuka zaidi.

Alisema kutokana na ukosefu wa walimu shuleni hapo imesababisha baadhi ya wanafunzi kuhitimu elimu ya msingi bila kujua vizuri kusoma na kuandika kwani amekuwa akitoa malalamiko ya kuomba walimu kwa wakuu wake wa kazi kwa muda mrefu bila mafanikio lakini mwaka huu 2015 ameongezwa mwalimu mmoja na anamuda wa wiki moja tokea aripoti hivyo bado hali ni ngumu licha ya kuwa tayari ameongezeka mwalimu huyo.

Mwalimu Shamimu aliiomba Serikali kuliangalia upya suala la mgao wa walimu hasa katika shule za vijijini zenye walimu wachache ambao wanafanya kazi ngumu kwani mishahara inayotolewa na Serikali haibagui kuwa huyu ni mwalimu wa kijijini na anatumia nauli kufuata mshahara na huyu ni mwalimu wa mjini hatumii nauli.

Akitolea ufafanuzi wa upungufu wa walimu kaimu ofisa elimu wa wilaya ya Ludewa Bw.Jimson Mgowole alisema mpaka sasa ni zaidi ya shule tatu zenye mwalimu mmoja kutokana na hali halisi ya wilaya ya Ludewa kuwa na upungufu mkubwa wa walimu hivyo kuifanya wilaya kushuka kielimu tofauti na wilaya nyingine za mkoa wa Njombe.

Bw.Mgowole alikili kuwepo kwa mwalimu mmoja kwa shule ya Kingole lakini alisema kuwa mpango wa Serikali na Halmashauri ya wilaya ya Ludewa ni kuhakikisha shule hiyo na nyingine zenye upungufu mkubwa wa walimu kuzipa mgao wa walimu wapya wanaotarajia kuletwa na wizara hivi karibuni kwani shule nyingi zilizoko mwambao wa ziwa Nyasa zina upungufu mkubwa wa walimu.

“Ni kweli kuwa shule za msingi mfano Kingole,Masi mavalafu,Nkwimbili,Ntumbati na nyingine zina mwalimu mmoja mmoja lakini tunachokifanya ni kuangalia awamu hii kipaombele zimepewa shule hizo ambazo zitapata walimu wapya lakini tatizo la ukosefu wa walimu katika wilaya yetu ni kubwa ndio sababu ya kushindwa kufanya vizuri katika sekta hii kwani mpaka sasa tuko katika asilimia 46 tu ya ufaulu tofauti na wilaya za wenzetu ndania ya mkoa wa Njombe”,alisema Bw.Mgowole.

Bw.Mgowole aliwataka wananchi kuwa watulivu kwani Serikali iko katika mchakato wa kuiboresha sekta ya elimu hivyo wanapaswa pia kuwatunza walimu wanaokwenda vijijijini hata hivyo alikiri kuwa na walimu wengi katika shule za mjini lakini alisema walimu hao ni wake wa viongozi wa wilaya na wengine ni wale wagonjwa wenye vyeti kutoka kwa madaktari vya kuwataka kukaa karibu na hospitari kubwa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Jumla ya Mara Iliyotazamwa