Jumamosi, 9 Mei 2015

Bilioni 8 Kutumika Kupanga Upya Jiji la Mwanza


SERIKALI inakusudia kutumia Sh bilioni nane katika mpango wake wa kulipanga upya Jiji la Mwanza kwa kuainisha sehemu za makazi, viwanda, biashara na huduma za kijamii.

Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Mkurugenzi Msaidizi wa Mpango Mkakati wa Kuyapanga Majiji kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mahenge Amulike, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau na viongozi wa Serikali wa sekta zote wa kupokea maoni na mapendekezo ya kuainisha maeneo hayo.
 
Pia aliwataka wakazi wa Mwanza na Arusha kutambua hakuna haja ya kumiliki  eneo kubwa la ardhi kwa ajili ya kujenga nyumba nyingi badala yake wanapaswa kumiliki eneo dogo ili kujenga ghorofa.

Alisema Serikali imeamua kuainisha maeneo ya majiji hayo kwa sababu ya ardhi kutoongezeka huku watu wakiongezeka kwa kasi hivyo ni lazima maeneo yakapangwa katika utaratibu unaotakiwa ikiwa ni kuepusha majanga yanatokana na watu kuishi katika maeneo hatarishi bila wao kujua.

Alisema tatizo kubwa lilipo kwa  Watanzania ni kutaka kumiliki eneo kubwa la kujenga nyumba kitendo kinachosabisha  watu wengine kukosa ardhi na kukosekana sehemu ya kuweka huduma za kijamii.

“Watu wanaongezeka kwa kasi lakini ardhi ipo pale pale tena mahitaji yanaongezeka, sasa bila kuyapanga majiji hayo kutakuwa na hatari mbeleni, lazima ardhi igawanywe kwa utaratibu unaokubalika, ni vema umiliki viwanja viwili kwa kujenga ghorofa 10 hadi 20 kuliko kumiliki ardhi kubwa na kujenga nyumba nyingi.

“Wapo watu wanaoishi milimani na mabondeni hao wapo hatarini, chukulia asilimia 70 ya wakazi wa Mwanza wanaishi milimani palipo na mawe, sasa jiwe la asili halitakiwi kuguswa au kuchimbwa lakini watu wamejenga nyumba juu ya mawe, ndiyo maana tunasikia yanaporomoka na hao maisha yao yapo hatarini,” alisema Amulike.

Alisema Serikali ya Tanzania ilisaini mkataba Januari 15 mwaka huu na watalaamu wa mipango miji kutoka Singapore ili kuyapanga majiji ya Arusha na Mwanza na ndani ya miezi 19 watashughulikia kuainisha na kupanga maeneo hayo.

Alisema baada ya kazi ya kuainisha kukamilika utaanza kutekelezwa na utakuwa na mkataba mwingine.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Jumla ya Mara Iliyotazamwa