Jumapili, 10 Mei 2015

Pinda: Tumedhamiria kuitokomeza malaria


WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda, amesema Serikali imedhamiria kumaliza tatizo la ugonjwa wa malaria kwa kuamua kujenga kiwanda cha kisasa cha kutengeneza dawa za kuua viluwiluwi wa mbu wanaosababisha ugonjwa huo.
 
Kiwanda hicho cha viua wadudu vya kuua viluwiluwi wa mbu wanaoeneza ungonjwa wa malaria, kimejengwa eneo la Tamco wilayani Kibaha, Mkoa wa Pwani.

Akizungumza baada ya kukagua kiwanda hicho juzi, alisema ana imani kujengwa kwa kiwanda hicho kutamaliza tatizo la malaria hapa nchini na katika nchi za jirani.

“Malaria ni ugonjwa hatari na unaongoza kwa kusababisha vifo hapa nchini. Watu karibu milioni mbili wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na ugonjwa huu. Tukianza kutengeneza hizi dawa zitasaidia kupunguza tatizo hili na kuokoa maisha ya watoto na wajawazito ambao ndiyo waathirika wakubwa.
 
 “Dawa hizi zinapotumiwa katika madimbwi, viluwiluwi ni lazima watakufa katika muda wa saa 24 na  katika dimbwi hilo dawa ile inabaki ikifanya kazi kwa muda wa mwaka mmoja.

"Hii ina maana wakizaliwa viluwiluwi wengine pia wanakufa bila hata kuweka dawa nyingine,” alisema Pinda.

Kiwanda hicho kitakachotoa ajira za moja kwa moja 186, kinatarajiwa kuzinduliwa Juni 25, mwaka huu na Rais Jakaya Kikwete na kinatarajiwa kuanza uzalishaji wa majaribio mapema mwezi ujao.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo, aliwaomba Watanzania kujenga viwanda vingi zaidi katika mkoa huo.

Akitoa maelezo kuhusu utengenezaji wa dawa hizo wakati Pinda akikagua kiwanda hicho, Msimamizi Mkuu wa Ujenzi, Dk. Ricardo Menendez, alisema ujenzi wa kiwanda hicho hapa nchini utatoa fursa kwa Tanzania kuuza dawa hizo kwa nchi za Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ambazo pia zinasumbuliwa na tatizo la malaria. 

“Tukishazalisha dawa za kutosha na kuzisambaza mikoa yote, itabidi tuangalie uzalishaji wa kibiashara kwa ajili ya nchi jirani zenye tatizo kama hili, hiki ni kiwanda pekee barani Afrika,” alisema Menendez.

Kiwanda hicho kinachojengwa kwa ushirikiano kati ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) na Kampuni ya Labiofamsa ya Cuba, kitakuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni sita za dawa ya ‘biolarvicides’ kwa mwaka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Jumla ya Mara Iliyotazamwa