MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi amevionya vyama vya siasa na wanasiasa wasikamiane na kukomoana kwa sababu, kufanya hivyo hakujengi demokrasia wala kuisaidia nchi.
Badala yake, amevielekeza viimarishe uelewano na kusaidiana, ili
kujenga Tanzania yenye amani na utulivu, hasa katika kipindi hiki cha
kuelekea katika uchaguzi mkuu.
Akizungumza Dar es Salaam jana wakati wa kufungua mkutano wa siku
mbili wa mashauriano ya jinsi ya kufikia na kuutekeleza uchaguzi mkuu wa
Oktoba kwa amani, Jaji Mutungi alisema ameona dalili za wanasiasa na
vyama vyao kukamiana.
Mkutano huo umeandaliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kwa
ushirikiano na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP),
litakalotoa ripoti ya utendaji wa ofisi hiyo katika mkutano
utakaoendelea leo jijini humo, lengo likiwa kuishauri namna ya kuboresha
utendaji.
Katika mkutano huo unaohusisha wadau mbalimbali wa siasa nchini,
wakiwemo wawakilishi wa vyama 22 vya siasa na taasisi tofauti, Jaji
Mutungi alisema, “Tanzania ina tunu ya amani, hivyo wanasiasa wasijaribu
kuivuruga kwa kuendesha siasa zisizo zingatia dhana ya demokrasia ya
kweli."
Alionya kuwa uzembe wowote utakaofanywa na wanasiasa au vyama vyao
unaweza kuiathiri nchi, na kuwafanya Watanzania wajute kuingia katika
mfumo wa siasa za vyama vingi.
Jaji huyo alisema pia kuwa amejiridhisha kuwa baadhi ya vyama vya
siasa vimeshindwa kuielewa vizuri dhana ya demokrasia ya vyama vingi,
hivyo kuwa na fikra za kukamiana na kukomoana, ambazo kwa namna yoyote,
hazimsaidii Mtanzania.
“Ninawaomba wanasiasa na vyama vyenu muelewe kuwa, harakati zote za
kufikia uchaguzi mkuu zinapaswa kuwa na lengo la kumtafuta kiongozi
atakayeiendesha nchi ifikie maendeleo.
“...Sote tunajenga nyumba moja
ambayo ni nchi yetu, hivyo, hatupaswi kugombania fito kwa mtindo
utakaosababisha nyumba isijengwe,”Jaji Mutungi alisisitiza na kuongeza
kuwa mikutano kama hiyo itaendelea kuwepo ili kupanua uelewa wa
wanasiasa juu ya dhana hiyo ya demokrasia ya vyama vingi.
Kwa upande
wake, Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP)
nchini, Philipe Poinsot aliipongeza Tanzania kwa kuendelea kukuza
demokrasia ya vyama vingi na kuwakumbusha wanasiasa na vyama vyao kuwa
wao ndio wenye dhamana ya kuilinda demokrasia hiyo pamoja na amani
iliyopo.
Alisema,”katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu,
Tanzania imekuwa na vuguvugu linaloweza kusababisha hali ya sintofahamu
kwa wananchi, jambo ambalo si jema hasa endapo nchi inaelekea kwenye
uchaguzi mkuu na matukio muhimu ya upigaji kura ya maoni."
Katika hatua nyingine, Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam (UDSM), Idara ya Sayansi ya Siasa, Dk Benson Bana alisema, ingawa
demokrasia ya vyama vingi inaonesha kuanza kufanikiwa nchini, vyama vya
siasa bado vinaitekeleza vikiwa na dhana ya utengano.
Mpekuzi blog
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni