Ijumaa, 10 Aprili 2015

WANANCHI LUFUMBU WAMPONGEZA DIWANI FARAJA MLELWA


 Diwani wa kata ya Mlangali Mh.Faraja Mlelwa

Hii ndiyo sola aliyoitoa kwa wananchi wa kijiji cha Lufumbu







Wananchi wakishangilia baada ya kukabidhiwa sola na Diwani Mlelwa


Wananchi wa kijiji cha Lufumbu kata ya Mlangali wilayani Ludewa katika mkoa wa Njombe wamempongeza diwani wa kata hiyo kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA  Mh.Faraja Mlelwa kwa kutoa msaada wa Sola katika Zahanati ya kijiji hicho ambapo awali walishindwa kupata huduma nyakati za usiku kutokana na kutokuwa na nishati ya umeme.

Akitoa shukrani hizo wakati diwani huyo akikabidhi sola hiyo Bi.Teresia Mtweve ambaye ni mjumbe wa serikali ya kijiji kupitia chama cha mapinduzi ccm alisema kuwa wagonjwa wamekuwa wakipata taabu nyakati za usiku hasa akina mama wajawazito kukosa huduma ya matibabu kutokana na kukosa umeme hivyo sola hiyo ni ukombozi mkubwa kwao.
Bi.Taresia alisema kuwa katika maendeleo hakuna suala la itikadi ya vyama vya siasa hivyo kata ya Mlangali imekuwa ikinufaika na mengi kupitia Diwani Mlelwa  kwani amekuwa ni mfano wa kuigwa katika utendaji wake hasa kwa kuwakumbuka akina mama na wazee ambao wanahitaji huduma ya Afya nyakati zote.
Alisema kuwa kukosekana kwa nishati ya umeme katika Zahanati hiyo kulisababisha wagonjwa hasa nyakati za usiku kusafiri hadi katika vijiji jirani ili kuweza kupata huduma za matibabu lakini hali ilikuwa mbaya zaidi pale msimu wa mvua unapofika na wagonjwa kushindwa kuwaishwa katika Zahanati jirani na mauti kuwafika wanaposhindwa kusafiri kutokana na mvua kubwa zinazonyesha nyakati za usiku.
“Tunamshukuru Mh.Mlelwa kwa kutusaidia hii sola maana itakuwa mkombozi kwetu hasa akina mama wajawazito kwani tumekuwa na shida sana wakati wa kujifungua hasa usiku waganga wanashindwa kufanya kazi na giza hali inayosababisha vifo kwa baadhi ya wagonjwa wa kawaida na akina mama kwa sasa hatutahangaika tena kutafuta bodaboda usiku kwani ikinyesha mvua ndio tatizo zaidi hatuwezi kusafiri”,alisema Bi.Teresia.
Naye mganga mkuu wa Zahanati ya Lufumbu Dkt.Wolfram Kiowi alisema kukosekana kwa umeme katika Zahanati hiyo kulisababisha baadhi ya Dawa kama chanjo ya Mama na Mtoto kutohifadhiwa hapo kwani majokofu ya kuhifadhi dawa hizo yanahitaji umeme hivyo kwa sasa dawa hizo zitahifadhiwa hapo na kuwawezesha wahitaji kupata huduma kwa urahisi zaidi.

Dkt.Kiowi alisema Mh.Faraja ameweza kuisaidia Zahanati hiyo kwa mambo mengi likiwemo la Dawa na Darubini ambavyo alivileta mapema mwaka 2014 na kufanya Zahanati hiyo kuendelea na upimaji wa vimerea vya magonjwa mbalimbali tofauti na awali wagonjwa walikuwa wakitibiwa kwa utabiri kwama waganga wa asili.
Alisema kata ya Mlangali inawasomi wengi kama Mh.Mlelwa hivyo wanapaswa kuwasaidia wananchi wa kata hiyo kama anavyofanya mwenzao kwani ameweza kuzisaidia Zahanati za vijiji vyote katika kata ya Mlangali kwa kutoa msaada wa Dawa na Darubini hivyo amekuwa mfano wa kuigwa na jamii inayomzunguka.
Aidha Diwani Mlelwa alisema katika uongozi wake ameweza kukamilisha ahadi zake zote alizowaahidi wananchi katika kampeni zake hivyo aliwataka wananchi kuvitumia vifaa hivyo kwa umakini ili viweze kuwanufaisha na watoto wa kizazi kijacho bila kubagua itikadi za vyama vya siasa.
Diwani huyo ambaye ni Diwani kijana katika Halmashauri ya wilaya ya Ludewa aliingia katika siasa mwaka 2012 mwishoni baada ya aliyekuwa diwani wa kata ya Mlangali kupitia chama cha mapinduzi kufa kwa kujinyonga na kamba hivyo ameweza kufanya kazi kwa miaka miwili na kukubalika kwa kiasi kikubwa na wananchi wa kata yake ambapo kata hiyo imeshagawanywa na kuwa kata mbili kwa sasa.
Mh.Mlelwa alisema katika Kampeni zake aliliona suala kubwa linaloisumbua kata ya Mlangali ni sekata ya Afya na elimu hivyo aliwaeleza wananchi kuwa ataanza na hayo licha ya kuwa ameweza kuungana na wananchi katika kuibua miradi mbalimbali ikiwemo ya maji lakini aliyoanza nayo ameweza kuyakamilisha kwa muda muafaka.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Jumla ya Mara Iliyotazamwa